Maafisa Wilaya wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) wameshiriki katika uangalizi wa Uchaguzi Mdogo wa Udiwani kwa upande wa Tanzania Bara ambapo wagombea 127 kutoka vyama 18 vya siasa wameshiriki katika Uchaguzi Mdogo wa Udiwani katika kata 22 za Tanzania Bara, Uchaguzi uliofanyika tarehe 20 Machi, 2024.

Akitoa pongezi zake kwa Tume ya Uchaguzi ya Taifa (NEC) na wananchi waliojitokeza katika Uchaguzi huo Afisa Uchaguzi Wilaya ya Magharibi ‘B’ Khadija M. Ali, wakati wa kutembelea
Vituo vya Kupigia Kura Kata ya Kimbiji Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni Mkoa wa Dar-es-Salaam alisema wadau wote wakiwemo wapiga kura na wananchi katika kata hiyo wamefanya Uchaguzi kwa utulivu mkubwa na mwitikio wa wananchi katika kata hiyo umekuwa wakuridhisha.

Sambamba na Hilo ameipongeza Tume ya Uchaguzi ya Taifa NEC kwa kuwapa mualiko huo kwani unaendeleza mashirikiano mazuri na mema baina ya Tume hizo mbili katika masuala ya kitaifa yanayohusiana na Uchaguzi.

Nae Issa Juma Hamad Msaidizi Afisa Uchaguzi Wilaya ya Micheweni ambae alitembelea vituo vya kupigia Kura katika kata ya Msangani Halmashauri ya Mji Kibaha Mkoa wa Pwani pamoja na Mahmoud Ahmada kutoka Wilaya ya Mkoani aliwashauri wananchi kuendelea kujitokeza kwa wingi kupiga kura ili kutimiza haki yao ya kuchagua viongozi wanaowataka katika Uchaguzi huo wa Madiwani.

“wito wangu kwa Wapiga Kura wajitokeze kwa wingi kwenda kupiga kura kwa ajili ya kuchagua madiwani wetu ambayo kila”

Aidha, aliwaomba Wapiga Kura kutekeleza jukumu hilo kwa utulivu na amani kwani kuna maisha baada ya Uchaguzi huo Mdogo.

Katika uangalizi huo Maafisa 4 wameshiriki katika Uchaguzi huo ambao ni Msaidizi Afisa Uchaguzi wa Wilaya ya Kati Said H. Vuai na Afisa Uchaguzi Wilaya ya Magharibi ‘B’ Khadija M. Ali, Issa J. Hamad kutoka Wilaya ya Micheweni na Mahmoud A. Mbwana kutoka Wilaya ya Mkoani Pemba,

ZEC na NEC zimekuwa zikishirikiana katika masuala mbalimbali ya Kiuchaguzi kwa mujibu wa Kifungu cha 119 (14) cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984.

 

 

Mfuko wa Huduma za Afya Zanzibar (ZHSF) imeendesha mafunzo ya siku moja ya kuwajenga uwezo na uelewa juu ya utoaji huduma wa Mfuko huo visiwani Zanzibar.

Mafunzo hayo ya siku moja yamefanyika katika ukumbi wa Afisi ya Tume ya Uchaguzi ya Wilaya ya Magharibi ‘A’ iliyopo Mwera nje kidogo ya jiji la Zanzibar  lengo likiwa ni kuwaandaa wadau muhimu katika  matumizi ya Mfuko huo nchini.

Akifungua mafunzo hayo Afisa Masoko na Uhusiano kutoka Mfuko wa Huduma za Afya Zanzibar (ZHSF)  Asha Kassim Mbiwi  alisema Mfuko huo umeanzishwa kwa mujibu wa Sheria Namba 1 ya mwaka 2023 ambayo ni   Sheria ya Mfuko wa Huduma za Afya Zanzibar,Sheria  ambayo ina umuhimu mkubwa nchini kwani inalenga katika kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora za afya kwa wote za uhakika na endelevu kwa wananchi na wakaazi wote wa Zanzibar na kuhakikisha upatikanaji wa rasimali fedha za kutosha na endelevu za kugharamia huduma za afya kwa wote hatua ambayo itaweza  kuweka mazingira bora ya kukuza na kustawisha huduma za Afya nchini.

Akizungumzia baadhi ya majukumu ya Mfuko huo alisema unajikita katika kulipia huduma za Afya kwa  wanachama na wategemezi wao,kukusanya, kuhifadhi na kusimamia michango ya wanachama pamoja na fedha nyengine zitakazolipwa na kulinda maslahi ya wanachama.

 Aliwakumbusha washiriki kuyatumia vyema mafunzo hayo ili kujijengea uelewa wakutosha  na uelewa sahihi wa Mfuko huo kwani wadau mbali mbali wamekuwa na maswali mengi juu ya Mfuko huo.

“kupitia mafunzo haya mtaweza kuuliza maswali ya kina pamoja na kutoa maoni yenu muhimu kuhusu huduma hii ili tuweze kuyazingatia na kuyatekeleza kwa maslahi ya wananchi wetu hapa Zanzibar  hasa nyinyi wafanyakazi wa Serikali ambao ni miongoni mwa makundi ya kwanza kufikiwa katika elimu hii ambayo ilianza kwa ngazi za juu za viongozi wa juu wa kila Taasisi za Serikali ya Zanzibar’’ alisema.

Aidha,  alisema wataendelea na program za kutoa elimu kwa Taasisi za Serikali hadi pale watakapokamilisha kutoa mafunzo kwa Taasisi zote za Serikali na zoezi kama hilo linafanyika Unguja na Pemba na zoezi kama hili litafanyika pia kwa wafanyakazi wa sekta binafsi.

Akitoa ufafanuzi juu ya maswali mbali mbali yaliyoulizwa katika mafunzo hayo Bi.Asha  alisema Mfuko huo bado haujawafikia Wazanzibar wote na umeanza kwa Wafanyakazi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar lakini malengo ni kuwafikia Wazanzibar wote na Mfuko huo unaamini kuwa taarifa muhimu kuhusu huduma hiyo mpya zitawafikia walengwa wote kote nchini,

Nae Afisa Uchaguzi Wilaya ya Kaskazini ‘B’ Bi Mwanamkuu Gharib Mgeni Alisema mafunzo hayo yamewapa faraja wafanyakazi wa Tume kwani wameelewa jinsi Mfuko unavyofanya kazi na walengwa wa Mfuko huo,na mafunzo hayo yamewanufaisha na kujua azma ya Serikali na muelekeo wake,amewaasa wafanyakazi kutoiacha fursa hiyo muhimu kwani huwezi kufanya kazi ukiwa huna afya bora.

Akitoa shukrani zake kwa niaba ya Wafanyakazi wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar Mkuu wa kurugenzi ya Huduma za Sheria ndugu.Maulid   aliwashukuru na kuwapongeza kwa kuwapatia mafunzo hayo juu ya Mfuko huo.

 

 

Tume ya Uchaguzi ya  Zanzibar (ZEC), imeandikisha jumla ya Wapiga Kura Wapya wapatao 57,883 katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa awamu ya kwanza. 

 

 Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa Tume hiyo Mhe.Jaji George J. Kazi alipofungua Mkutano wa Tathmini ya Uandikishaji wa Wapiga Kura Wapya kwa awamu ya kwanza, uliofanyika katika ukumbi wa Sheikh Idriss Abdulwakil Kikwajuni Mjini. 

Alisema kuwa miongoni mwa hao walioandikishwa wanawake ni 31,440 na wanaume ni 26,443  huku Watu Wenye Ulemavu walioandikishwa ni 1,280.

Aidha, alisema kuwa hatua ya Uandikishaji imekamilika na Tume inatarajia kuweka wazi orodha  ya Wapiga Kura hao katika vituo vyote vilivyotumika kwa Uandikishaji wa Unguja na Pemba kwa muda wa siku saba kuanzia  Machi 1 hadi 7 mwaka huu. 

Alifahamisha kwamba kazi hiyo inafanyika kwa mujibu wa maelekezo ya kifungu cha 19(1) cha Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar namba 4 ya mwaka 2018 , ambacho kinamtaka Afisa wa Uandikishaji, kutayarisha na kuweka wazi orodha ya Wapiga Kura walioandikishwa kwa muda wa siku hizo katika eneo la wazi la Afisi ya Wilaya au eneo jengine lolote litakaloamuliwa na Tume. 

Aidha alisema sambamba na uwekaji wa wazi wa orodha ya Wapiga Kura Wapya, Tume itaweka wazi orodha ya Wapiga Kura walioomba kuhamisha taarifa zao kutoka eneo moja kwenda eneo jengine la Uchaguzi. 

Alifahamisha kwamba madhumuni ya kufanya  hivyo ni kutoa nafasi kwa muombaji alieandikishwa kuwasilisha malalamiko ya kurekebisha taarifa zake,  kuomba jina lake liingizwe katika orodha iwapo aliandikishwa lakini hakuorodheshwa au kuweka pingamizi dhidi ya taarifa za muombaji mwengine aliekatika orodha.

Hata hivyo alisema kuwa kufanya hivyo kutawawezesha kujua kama taarifa zao zimo  katika orodha au kujua iwapo taaarifa zao zimenakiliwa kwa usahihi au kuweka pingamizi kwa wasio na sifa. 

Hivyo aliwaomba Wadau wa Uchaguzi na wananchi kwa ujumla kuwahamasisha vijana walioomba kuandikishwa kwenda kuangalia taarifa zao, kwani kufika kwao vituoni kuangalia taarifa kutawahakikishia nafasi ya kuwemo katika Daftari na kuwa Wapiga Kura. 

Akitoa taarifa ya Tathmini ya zoezi hilo Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi ndugu.Thabit Idarous Faina alisema kuwa Tume ilitarajia kuandikisha Wapiga Kura Wapya 162,606.

Hata hivyo alisema pamoja na kuonekana idadi hiyo ni ndogo  lakini wamefikia malengo yao ukilinganisha na Uandikishaji wa miaka uliopita.

Akitoa Tathmini ya Uandiskishaji kiwilaya Faina alisema kuwa Wilaya ambayo imeandikisha watu kidogo ni Mkoani iliyoandikisha watu 2,562 sawa na asilimia 21.41 ambapo walitarajia kuandikisha Wapiga Kura Wapya 11,964 ikifuatiwa na Wilaya ya Micheweni iliyoandikisha watu 2,628 kati ya 10,907 sawa asilimia 24.09 ya waliokuwepo katika matarajio ya kuandikishwa. 

Wilaya nyengine ni Wilaya ya Magharibi ‘A’ walioandikishwa ni 7,157 kati ya 28,677 sawa na asilimia 24.96  huku Wilaya ya Kusini imefikisha asilimia 60 kwa kuandikisha watu 2,875 kati ya 4,792 , Wilaya ya Kaskazini ‘A’ imeandikisha watu 7,265 kati ya watu 13,169 sawa na asilimia 55.17 na Wilaya ya Mjini imeandikisha watu 10,722 kati ya watu 19,272 sawa na asilimia 55.64%

Kwa upande wake Mkuu wa Kurugenzi ya Huduma za Uchaguzi Khamis Issa Khamis akizungumzia kuhusu zoezi la uwekaji wazi orodha ya Wapiga Kura na walioomba kuhamisha taarifa zao alisema, hadi kufikia Febuari 14, mwaka huu, jumla ya Wapiga Kura 302 wamewasilisha maombi ya kuhamisha taarifa zao kutoka eneo moja kwenda jengine la Uchaguzi. 

Hata hivyo alisema kuwa uhamisho wa taarifa za Wapiga Kura ni endelevu na kazi ya kupokea taarifa za wanaoomba kuhamisha inaendelea kufanyika katika Ofisi za uchaguzi za Wilaya kila siku kwa saa za kazi. 

Nao washiriki wa Mkutano huo wakiwemo viongozi wa vyama vya Siasa waliishukuru Tume kwa kuwashirikisha katika kila eneo la zoezi hilo ikiwemo upatikanaji wa  mawakala lakini changamoto ambayo wameipata ni kukosa fursa ya kushuhudia zoezi hilo. 

Hivyo waliiomba Tume hiyo kwa zoezi la Uandikishaji la awamu ya pili wapatiwe nafasi hiyo, suala ambalo lilitolewa ufafanuzi na Mkurugenzi wa Uchaguzi Thabit Idarusi Faina ya kuwa haliwezekani, kutokana Sheria ya Tume ya Uchaguzi haijaruhusu mwanasiasa kuingia katika vyumba vya Uandikishaji na badala yake kuwaweka mawakala wao.

 

 

Wanasiasa watakiwa kubadilika na kuwa wakweli  ili kuepuka kuopotosha Umma

Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) Mhe.Jaji George J. Kazi amewataka Wanasiasa kubadilika na kuwa wakweli wanapoeleza  shughuli zinazofanywa na Tume hiyo ili kuepusha siasa za Uchochezi na hatimae kuibakisha nchi ikiwa salama.

Alisema kuendelea kuwapa habari wananchi zisizo na ukweli ni sawa na upotoshaji kwani mambo yote yanayoendeswa na Tume hayafichwi yako wazi na kila mmoja anaona na wadau mbali mbali wamekuwa wakishirikishwa katika kazi za ZEC ikiwemo Uandikishaji Wapiga Kura.

Jaji Kazi, alieleza hayo huko katika ukumbi wa ZSSF Tibirinzi Chake Chake Pemba katika Mkutano wa Tathmini ya zoezi la Uandikishaji Wapiga Kura Wapya kwenye Daftari la kudumu  lililoendeshwa na Tume hiyo kwa Mikoa yote ya Zanzibar kuanzia tarehe  2 Disemba  2023 hadi tarehe 15 Januari 2024.

Alisema kuwa wakati wa Zoezi la Uandikishaji likiendeshwa viongozi wote wa Tume hiyo walikuwa wakifuatilia na kulikuwa na mashirikiano makubwa baina ya watendaji na Mawakala wa Vyama vya Siasa ,hivyo dosari yoyote ilikuwa inajitokeza ilikuwa inapatiwa ufumbuzi wa haraka ili kuhakikisha kila mwananchi anapata haki yake hiyo.

“ Watendaji wote wa Tume hii walikuwa hawakai Ofisini kuanzia mwanzo wa zoezi mpaka mwisho wa zoezi hivyo changamoto zote ambazo zilikuwa zinajitokeza katika zoezi hilo zilipatiwa ufumbuzi wa pamoja na nichukuwe fursa hii kuwapongeza wadau wote kwa ushirikiano wenu mulioipatia Tume yetu”, alisema.

 

 

Akizungumzia kumalizika kwa zoezi hilo Mwenyekiti huyo alifahamisha kuwa zoezi lilikwenda vyema kwa Amani na utulivu.

Alisema katika zoezi hilo jumla ya Wapiga Kura Wapya  57,883wameandikishwa wakiwemo Wanawake 31,440 na Wanaume 26,443 sawa asilimia 35.6 ya walioandikishwa ingawaje matarajio ni kuandikisha Wapiga Kura Wapya 162,606, lakini pamoja na zoezi hilo kumalizika kazi inayofuata ni kuweka wazi Daftari kwa muda wa siku saba kuanzia tarehe 1 hadi 7 Machi 2024.

Aliwataka Wadau wa Uchaguzi na wananchi kwa ujumla kuwahamasisha Vijana waliomba kuandikishwa kwenda vituoni kuangalia taarifa zao kwani kufika kwao vituoni kuona taarifa zao kutawarahisishia nafasi ya kuwemo katika Daftari na kuwa Wapiga Kura.

“ Tume inawaomba Wananchi  muendelee kudumisha Amani na utulivu ndani ya nchi yetu na kutoa ushirikiano mzuri kwa shughuli zinazoendeshwa na Tume ya Uchaguzi Zanzibar katika mzunguko wote wa Uchaguzi”, alisema.

Akitoa Tathmini ya Wapiga Kura wapya awamu ya kwanza Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar , Thabit Idarous Faina alisema kuwa kifungu cha 19 ( 1) cha Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2018 kinaelekeza afisa Uandikishaji baada ya kukamilika kwa Uandikishaji Wapiga Kura kwa kufuata miongozo ya Tume ataweka wazi orodha ya waombaji wapya katika kila kituo cha Uandikishaji kwa muda wa siku 7.

Alifahamisha sambamba na hilo pia kifungu cha 19 (2) kinaeleza kuwa Mpiga Kura yoyote au muombaji anaweza kuchunguza orodha ya Wapiga kura  iliowekwa wazi kwa madhumuni ya kuthibitisha kuwa yumo, kuangalia usahihi wa taarifa zake au kuweka pingamizi taarifa za muombaji mwengine asiekuwa na sifa katika orodha hiyo.

Alieleza kuwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) kwa mujibu wa mpango kazi wake itaendesha zoezi kama hilo kwa awamu ya pili kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka  2025.

“ Niwahakikishie wadau Uchaguzi kuwa shuguli zote zinazofanywa na Tume hii zinakwenda kwa mujibu wa Sheria na sio kwa matakwa ya watu wengine “, alisema

Alifahamisha kuwa wakati wa zoezi hilo wadau mbali mbali walishirikishwa na Tume kuanzia ngazi ya mwanzo hadi ya mwisho kwa mujibu wa nafasi zao wakiwemo  Vyama vya Siasa, vikosi vya Ulinzi na Usalama, asasi za kijamii Vyombo vya habari , makundi maalumu nakadhalika.

Mkurugenzi huyo alisema katika kufanikisha zoezi hilo kwa mujibu wa Sheria namba 4 ya mwaka 2018 , kifungu cha 14 (1) Vyama vya Siasa viliruhusiwa kuweka Mawakala wao katika vituo vyote vya Uandikishaji ili kuangalia mwenendo wa Uandikishaji ambapo jumla ya Vyama 14 viliweka Mawakala wao.

Alieleza vyama 5 vya siasa havikuweka Mawakala wao katika zoezi hilo kwa sababu zao mbali mbali, aidha asasi za kiraia 10 zilishiriki zoezi hilo .

Aliwapongeza wadau wote wa Uchaguzi kwa ushiriki wao katika kufanikisha zoezi hilo na kuwataka waendelee kudumisha Amani na utulivu kwani ndio uliowezesha kufanyika kwa kazi hiyo muhimu ya Kidemokrasia.

Nae Mkurugenzi wa Huduma za Uchaguzi kutoka Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) ndugu Khamis Issa Khamis alisema mpaka kufikia tarehe 15 Febuari mwaka 2024 jumla ya wapigakura 323 wameshawasilisha maombi ya kuhamisha taarifa zao kutoka eneo moja kwenda jengine la Uchaguzi.

Alieleza kuwa uhamisho wa taarifa za Wapiga kura ni endelevu  na kazi ya kupokea taarifa za wanaoomba kuhamisha inaendelea kufanyika katika Afisi za Uchaguzi za Wilaya kila siku kwa saa za kazi.

Hata hivyo Tume inawasisitiza wananchi kudumisha Amani na Utulivu wakati wa zoezi la kuangalia taarifa zao sambamba na kutowa ushirikiano mkubwa ili zoezi liende vizuri.

 

           

 

Leo tarehe 24 Januari 2024 Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar Ndugu Thabit Idarous aliikaribisha Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi inayotathmini utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo na programu mbali mbali za Serikal ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mwanaasha Juma Khamis ambae ni Muwakilishi wa Jimbo la Dimani, kamati hiyo imetembelea mradi wa Ujenzi wa Afisi Kuu ya Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) Maisara,Mjini Unguja ulioanza rasmi tarehe 11 Januari mwaka huu na unatarajiwa kukamilika kwa kipindi cha miezi 9.

Ujenzi huo unasimamiwa na Kampuni ya Ujenzi ya CRJE kutoka China ambapo watajenga jengo la kisasa lenye Ghorofa nne ambazo zitajumuisha kumbi mbali mbali za Mikutano ikiwemo Ukumbi wa kutangazia matokeo ya Uchaguzi, Studio ya Redio na TV, Ghala la Kuhifadhia Vifaa vya Uchaguzi N.k

Jengo hilo linatarajiwa kuwa la Kisasa zaidi kuendana na hadhi ya Afisi za Tume nyengine Duniani.

 

Mawasiliano Yetu


Tume ya Uchaguzi Zanzibar

S.L.P 1001 - Zanzibar, Tanzania.

Simu: +255 242231489

Nukushi: +255 242233828

Mitandao ya Kijamii