NA  AHMED A. MOHAMMED-ZEC

Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar  imetoa mafunzo ya nadharia na vitendo  kwa wanafunzi wa shule ya Sekondari ya DKT.Salim Ahmad Salim kwa lengo la kuwajengea uelewa juu ya zoezi zima la Uchaguzi unavyofanyika.

Mafunzo hayo yametolewa na  Maafisa kutoka Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar Kisiwani Pemba siku ya Alhamis ya tarehe 17/08/2023 katika skuli hiyo iliyopo Chakechake Shehia ya Wara Kisiwani  Pemba,ambapo  wanafunzi 641 na walimu wa skuli hiyo walishiriki mafunzo hayo,ikiwa pia ni maandalizi ya Uchaguzi wa Serikali ya Wanafunzi wa Skuli hiyo,Uchaguzi ambao ulifanyika siku ya Ijumaa ya Tarehe  18/08/2023 majira ya saa 3:30 za Asubuhi.

Akifungua mafunzo hayo Afisa Uchaguzi  Wilaya ya Chakechake Ndugu.Abdallah  Juma Abdallah na Ndugu.Juma Mkubwa Issa ambae ni Afisa elimu ya Wapiga Kura Pemba amesema lengo la mafunzo hayo kwa wanafunzi ni kuwapatia  uelewa ili wapate kuyatambua  majukumu mbali mbali ya Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar  na namna ya Uchaguzi unavyoendeshwa, elimu ambayo itawawezesha kushiriki vyema katika ujenzi wa utawala bora.

Aidha,aliwaeleza wanafunzi  hao  elimu  juu  ya  mwenendo  mzima wa Uchaguzi na Kura ya Maoni inavyofanyika ili kuwasaidia wanafunzi kuelewa juu ya namna ya uteuzi wa Serikali unavyofanyika ikiwemo Serikali mbili,tatu au Serikali ya umoja wa kitaifa,kuanzia mchakato mzima wa maoni hadi siku ya Uchaguzi  ambayo wananchi huchagua viongozi wanaowataka,

Nae  ndugu. Juma Mkubwa ambae ni Afisa Elimu wa Tume hiyo Kisiwani Pemba licha ya kutoa elimu juu ya masuala mbali mbali ikiwemo zoezi zima la kugombea nafasi mbali mbali wakati wa Uchaguzi pia aliwapa  wanafunzi hao  nafasi ya kuuliza na kujibu maswali mbali mbali  ili kupima uelewa wao wakati wa utoaji wa mafunzo kwa wanafunzi hao.

Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa Skuli hiyo ndugu.Khamis Said Othman aliwaasa Walimu na Wanafunzi ambao wameshiriki katika mafunzo hayo kuipokea elimu hiyo ya dhana nzima ya Uchaguzi kwani tukio hilo limebeba mazingatio makubwa kwa maisha yao ya sasa na baadae.

 Nae Rais mstaafu wa Serikali ya Wanafunzi wa Shule hiyo  Mustafa Kassim ameishukuru Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar  kufika Shuleni kwao na kuwapatia mafunzo hayo kwani yatawasaidia katika kuzitambua haki zao na kuyatambua masuala mbalimbali ya kisiasa.

Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar imekuwa ikishirikiana na Taasisi mbali mbali Binafsi na za Serikali katika kuzipatia mafunzo  ya  Elimu ya Mpiga Kura. 

 

Mawasiliano Yetu


Tume ya Uchaguzi Zanzibar

S.L.P 1001 - Zanzibar, Tanzania.

Simu: +255 242231489

Nukushi: +255 242233828

Mitandao ya Kijamii